Tuesday

ROMA AFUNIKA TAMASHA LA WASHINDI WA KILI MBEYA

On Streets Today
Msanii AT kutoka Zanzibar akitumbuiza jukwaani na wacheza shoo wake wakati wa onyesho maalum la Washindi wa Kili Music Awards jijini Mbeya kwenye Uwanja wa Sokoine juzi. (Picha: Mpigapicha Wetu)

Nyota wa hip hop nchini, Roma Mkatoliki, aliacha gumzo mjini Mbeya wakati alipofanya shoo ya uhakika na kuamsha shangwe mpya, licha ya kuwa msanii wa pili kutoka mwisho katika ratiba ya watumbuizaji wa onyesho la ziara ya washindi wa tuzo za Kilimanjaro kwenye Uwanja wa Sokoine juzi.
Mashabiki waliimba jina lake tangu msanii huyo alipoitwa stejini na alipofika hakuwaangusha.
Alitumbuiza kwa nyimbo zake kali na wakati mashabiki wakidhani kwamba shoo yake imefikia tamati, rapa huyo alisema: "Sasa ndugu zangu, nawaambia ukweli kwamba kufikia muda huu mmetumia Sh. 200 tu ya kiingilio chenu... sasa nawapa shoo ya Sh. 1,800 iliyobaki.”
Huku mashabiki wakishangilia kwa nguvu, Roma alimalizia kwa kuimba wimbo wa Mathematic uliompa tuzo.
Wasanii wengine waliopanda stejini ni pamoja na Ben Pol, AT, Ali Kiba, Barnaba, Ommy Dimpoz na Suma Lee ambao nao walifanya shoo ya uhakika.
Mshindi wa tuzo ya wimbo bora wa R&B, Ben Paul ambaye alijinyakulia tuzo hiyo kupitia wimbo wake wa 'Number One', alifungua jukwaa na kuwaamsha watu kuwa sasa shoo imeanza.
Alifuata jukwaani Suma Lee ambaye aliongozwa na shoo kali kutoka kwa vijana wake wanne wa kike na wa kiume na kushangiliwa vilivyo.
Kisha alipanda mkali kutoka Zanzibar ambaye ni mshindi wa Tuzo Wimbo Bora wenye Vionjo vya Kiasili, Ally Tall a.k.a AT na kutoa burudani ya nguvu na wimbo wa 'Vifuu Tundu' akiwa na wanenguaji wake wawili wa kike.
Nyota wa wimbo 'Baadaye', Ommy Dimpoz alipanda jukwaani na kutumbuiza kwa wimbo huo pamoja na 'Nai Nai' uliompa tuzo ya Wimbo Bora wa Kushirikiana aliomshirikisha Ali Kiba.
Ali Kiba alibaki jukwaani hapo kama ilivyokuwa mjini Moshi na vijana wake kumfuata kutoa shukrani zao za kupata kura zilizowapa ushindi wa tuzo ya Wimbo Bora wa Zouk Rhumba kupitia wimbo wa 'Dushelele'.
Mshindi wa Tuzo ya Mwimbaji Bora wa Kiume, Barnaba ndiye aliyefunga pazia hilo mjini Mbeya kwa kuimba wimbo wake unaotamba sasa wa 'Magube Gube'.
Wasanii hao wiki ijayo wanataraji kutoa burudani kama hiyo jijini Mjini Mtwara, baada ya kuwa tayari walishatumbuizakatika miji ya Dodoma, Mwanza na Moshi.

MAKALA ATOA MAMILIONI KWA UJENZI WA MASOKO YA KISASA

On Streets Today
Naibu Waziri wa Habari,Vijana,Utamaduni na Michezo Amos Makalla
Naibu Waziri wa Habari,Vijana,Utamaduni na Michezo Amos Makalla,ametoa shilingi milioni 20 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa masoko katika kata ya Mvomero, Dakawa, Mlali na Kibati wilayani Mvomero Mkoani Morogoro.
Makalla ambaye ni Mbunge wa Jimbo hilo amekabidhi hundi za Sh. milioni 5 kwa kila kata ili kuwezesha kuanza kwa mchakato wa ujenzi wa masoko ya kisasa katika maeneo yaliyotengwa  wakati wa ziara yake ya kukagua na kuhimiza maendeleo kwa wananchi wa wilaya hiyo.
Mbunge huyo alitaka  mpango wa ujenzi wa masoko hayo  uanze kufanyika mara moja ikiwa na kuweka  makadiriko ya gharama za ujenzi.
Kata ya Mvomero ilikuwa ya kwanza  kukabidhiwa wakati wa   mkutano  wa hadhara uliofanyika hivi karibuni   na pia kuuagiza uongozi wake kuanza mchakato wa ujenzi wa soko la kisasa litakaotumiwa na wananchi wa ndani na nje ya kata ili kwenda na kasi ya ukuaji wa mji huo.
Aliwataka wananchi kwa kushirikianana uongozi wao na nguvu za Mbunge atakapofikisha hatua nzuri ya ujenzi itakuwa ni  rahisi kuwashawishi wadau wengine kuchangia ujenzi huo  pamoja na  Halmashauri ya Wilaya kutenga  bajeti ya fedha za kuendeleza ujenzi huo.
“ Huu ni mkakati wangu  na ni miongoni mwa kero zilizotolewa na wananchi juu ya ukosefu wa masoko “ alisema Mbunge huyo .
Mbunge huyo alitoa hundi za kiwango kama hicho kwa viongozi wa Serikali ya  Kata ya Kibati, Dakawa na Mlali na kusema masoko hayo yakikamilishwa yatawanufaisha wakulima na wananchi katika mifumo mizuri ya   bei  ya mazao .
Hata hivyo aliwaonya Viongozi wa Serikali za Vijiji  na Kata hizo ,kuwa fedha hizo zisitumiwe katika shughuli nyingine kinyume na ilivyokusudiwa na viongozi watakaokiuka utaratibu watawajibishwa.

LEMA ABOMOA KWA MAGUFULI

On Streets Today
Aliyekuwa Mbunge wa Arusha Mjini, Godbress Lema (Chadema)

Aliyekuwa Mbunge wa Arusha Mjini, Godbress Lema (Chadema), amezidi kuzisambaratisha ngome za Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli, baada ya makada saba wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Jimbo la Chato katika mkoa mpya wa Geita kukihama chama hicho na kujinga na Chadema.

Wakati tukio hilo likitokea, Lema, alielezea kushangazwa na uwezo mkubwa wa waziri huyo katika kutambua wingi wa samaki walioko majini pamoja na mimba zao, lakini ameshindwa kutatua tatizo la upatikanaji wa maji safi na salama kwa wananchi wa jimbo lake.

Akizungumza na wananchi wa Jimbo la Chato kwenye mkutano wa hadhara, Lema alimtupia lawama Dk. Magufuli kuwa ameshindwa kuwatumikia wananchi wake katika kutatua matatizo yanayowakabili ikiwemo ukosefu wa maji safi na salama.

Alisema wananchi hao wamekuwa wakitumia maji yasiyofaa kwa matumizi ya binadamu kutokana na kutumiwa na mifugo na wengine kuchota maji machafu ya ziwa ambayo yamekuwa yakiwasababishia magonjwa ya kuhara.

“Ndugu zangu inasikitisha sana kuona Chato ndiyo hii…wakati nikipita njiani kuja huku nimeshuhudia ziwa likiwa karibu kabisa na makazi yenu kiasi kwamba mbunge wenu angekuwa na nia thabiti ya kuwatumikia, nina imani wananchi wa hapa msingelikuwa masikini wa kutupwa namna hii…mimi ni mara yangu ya kwanza kufika hapa, lakini kutokana na mbwembwe za Magufuli bungeni kuonyesha anafahamu aina, idadi na mimba za samaki waliomo ndani ya maji niliamini Chato inafanana na Arusha kumbe la,” alisema.

Kauli hiyo ilisababisha wananchama 27 wa CCM wakiwemo makada saba kukihama chama hicho na kujiunga na Chadema, hatua iliyotofasiriwa kuwa ni kuendelea kuvunjwa ngome za Magufuli ambaye pia ni Mbunge wa Chato kutokana na nafasi nyingine za wenyeviti wa vijiji vinane kati ya 11 kutwaliwa na Chadema katika uchaguzi mdogo wa kuziba nafasi zilizokuwa zimeachwa wazi na viongozi waliokuwepo awali.

Baadhi ya makada wa CCM waliokihama chama hicho ni aliyekuwa Mwenyekiti wa Kijiji cha Mkuyuni Uhuru Selemani na aliyekuwa katibu wa vijana wa Kata ya Chato, Masumbuko Kaitila.

Masumbuko pia aliwahi kuwa mjumbe wa Baraza Kuu la UVCCM mkoa wa Kagera, mjumbe wa Kamati ya Utekelezaji mkoa wa Kagera na Katibu wa Hamasa wa Chipukizi Wilaya ya Chato.  Makada wengine mashuhuri waliohamia Chadema ni Lusia Kahindi, Fikiri Makoye, Samwel Mkome, Emmanuel Kayila na Vigoro Lucas.

Huku akitumia kauli mbiu ya “vua gamba vaa gwanda” na “vua ukada vaa ukamanda”, Lema aliwataka watumishi wa serikali hususani Jeshi la Polisi kuacha kutumia nafasi zao vibaya kwa kuwanyanyasa wananchi wakiwemo viongozi wa Chadema.

Alisema baadhi ya askari polisi wamekuwa wakitumiwa vibaya na viongozi wa chama tawala kutokana na kushinikizwa kuwapiga kwa marungu, mabomu na kuwabambikiza kesi baadhi ya wananchi na wafuasi wa vyama vya upinzani wakiamini kuwa njia hiyo itasaidia kudidimiza kasi ya mageuzi kwa jamii, hatua ambayo imekuwa ikiongeza chuki kwa wananchi dhidi ya polisi na serikali yao.

Aidha, aliwataka wananchi kwa kushirikiana na viongozi wa Chadema kushirikiana kufanya maandamano ya amani kuishinikiza serikali kuwafukuza kazi watendaji wabovu na wabadhirifu wa fedha za miradi ya maendeleo ya wilaya ya Chato ambazo zimedaiwa kutafunwa ili serikali iwaburuze mahakamani.

 MBOWE, SLAA KUONGOZA OPERESHENI KUSINI

Awamu mpya ya operesheni ya Chadema inayolenga kuhamaisha umma kuleta mabadiliko na uwajibikaji serikalini iliyopangwa kufanyika katika mikoa ya Kanda ya Kusini, itaanza rasmi Mei 28, mwaka huu, katika Mkoa wa Mtwara.

Akizungumza na NIPASHE jana, Mkurugenzi wa Habari na Uenezi wa Chadema, John Mnyika, alisema operesheni hiyo itaongozwa na Mwenyekiti wa chama hicho Taifa, Freeman Mbowe.

Alisema wengine watakaoongoza operesheni hiyo, ni Katibu Mkuu wa Chadema, Dk. Willibrod Slaa pamoja na wabunge wa chama hicho na kwamba, itahitimishwa katika mkoa wa Lindi.

Kwa mujibu wa Mnyika, operesheni hiyo imelenga kushughulikia mambo matatu; la kwanza likiwa ni kusimamia uwajibikaji katika ngazi zote za serikali, ili kuhakikisha changamoto zote zinazolikabili taifa zinashughulikiwa.

Mnyika ambaye pia ni Mbunge wa Ubungo, alisema jambo la pili litakaloshughulikiwa na operesheni hiyo, ni kutoa elimu ya kisiasa kwa umma kuhusu mchakato wa mabadiliko ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Alisema jambo la tatu, litakuwa ni kujenga organaizesheni ya chama mijini na vijijini katika mikoa hiyo.

Waliotemwa uwaziri waingia uso kwa uso na Takukuru

On Streets Today
  Asilimia 90 wamekwisha kuchukiliwa maelezo
Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru, Dk. Edward Hoseah

Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), imeshawahoji asilimia 90 ya Mawaziri wanaotuhumiwa kwa ubadhirifu wa fedha  za umma katika wizara zilizotajwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG).

Akizungumza na NIPASHE ofisini kwake jana, Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru, Dk. Edward Hoseah, alisema baadhi ya mawaziri waliotuhumiwa wamekwisha kuhojiwa na uchunguzi bado unaendelea dhidi yao.

Hata hivyo, Dk. Hoseah, alisema suala la kuwachunguza mawaziri hao siyo la kukurupuka kama baadhi ya watu wanavyofikiri kwani lazima lichukue muda kwa kuwa wanaangalia mambo mbalimbali ikiwemo haki za binadamu.

Alisema mapambano dhidi ya rushwa yanahitaji utashi wa kisiasa na taasisi yake inafanya kazi bila ya kuingiliwa na jitihada za kuunga mkono mapambano dhidi ya rushwa zimeonekana.

Mawaziri hao ambao waliachwa katika baraza la mawaziri  lililotangazwa na Rais Jakaya Kikwete Mei 4, mwaka huu, jana NIPASHE liliwatafuta kwa simu kuulizwa kama wamehojiwa na Takukuru na kujibu ifuatavyo:

MKULO


Mmoja wa mawaziri aliyetemwa ni Mustafa Mkulo (Fedha): “Mimi sina habari hiyo, si msemaji wa Takukuru, waulize wenyewe Takukuru.”

MAIGE

Waziri mwingine aliyetemwa, ni Ezekiel Maige (Maliasili na Utalii): “Sizungumzi sasa hivi na vyombo vya habari.”

Alipotakiwa kueleza sababu za kutozungumza na vyombo vya habari, Maige ambaye ni Mbunge wa Msalala (CCM), hakujibu, badala yake alisema hana habari zozote za kueleza iwapo alihojiwa na Takukuru au la.

“Habari hiyo sinayo, lakini sizungumzi na vyombo vya habari, ahsante,” alisema Maige kisha akakata simu.

NUNDU

Aliyekuwa Waziri wa Uchukuzi, Omar Nundu, alipopigiwa simu yake ya mkononi, alipokea na mwandishi alijitambulisha, lakini kabla hajaulizwa swali, alisema: “Siongei na mtu wa magazeti tafadhali. Kwa heri. Ahsante.” kisha akakata simu.

NGELEJA


Hata hivyo, wakati mawaziri hao walioachwa wakisema hayo, hadi tunakwenda mitamboni, simu ya aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja, mara zote ilipopigwa ilikuwa ikiita bila kujibiwa.

DK. CHAMI

Pia aliyekuwa Waziri wa Viwanda na Biashara, Dk. Cyril Chami, alipopigiwa, mara zote simu yake iliita, lakini haikujibiwa na baadaye ikazimwa kabisa.

DK. NKYA

Aliyekuwa Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Lucy Nkya, alisema: Sijawahi kupokea simu wala barua kutoka Takukuru kwenda kuhojiwa.”

DK. MFUTAKAMBA, DK. MPONDA


Aliyekuwa Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Haji Mponda na Naibu Waziri wa Uchukuzi, Dk. Athumani Mfutakamba  simu zao jana zilizimwa kabisa.

Ripoti ya CAG na taarifa za  kamati za kudumu za Bunge za Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC), Hesabu za Serikali (PAC) na Serikali za Mitaa (LAAC) ziliwataja baadhi ya mawaziri kuhusika katika ufujaji wa fedha za umma na wengine kushindwa kusimamia wizara na taasisi zao na kuisababishia serikali hasara.

Pia ripoti ya Kamati ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Mazingira, ilimtuhumu Maige katika mchakato wa kugawa vitalu vya uwindaji wa kitalii, akidaiwa kuruhusu kampuni ambazo hazikuomba vitalu kupewa kinyume cha sheria na kanuni na usafirishaji wa wanyama hai nje ya nchi.

Mkulo anadaiwa kuhusika katika ubadhirifu wa Shirika Hodhi la Mali za Mashirika ya Umma (CHC). Alitajwa kuwa amepoteza uaminifu na uadilifu kiasi cha kusema uongo bungeni ili kuficha maslahi binafsi katika ofisi za umma.

Dk. Chami, alitajwa kuhusika katika kumkingia kifua aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Viwango la Taifa (TBS), Charles Ekelege, kutokana na kusema uongo katika kazi ya ukaguzi wa magari nje ya nchi.

Ekelege anadaiwa kusema uongo kuwa kuna kampuni zimepewa kazi ya kukagua magari yanayokuja nchini nje ya nchi, ambayo yanalipwa mamilioni ya fedha, lakini kamati ya wabunge iliyokwenda nchi za Singapore na Hong Kong, hawakukuta kampuni hizo.

Mwishoni mwa wiki Waziri wa Viwanda na Biashara, Dk. Abdallah Kigoda, alitangaza kumsimamisha kazi Ekelege kupisha uchunguzi dhidi yake.

Dk. Mponda anadaiwa kushindwa kusimamia matumizi bora ya fedha za umma kiasi cha kuruhusu nyumba yake kukarabatiwa kwa mamilioni ya fedha.

Ngeleja, anatuhumiwa kwa kushindwa kusimamia sekta ya madini na umeme, kuweko kwa manunuzi makubwa ya mafuta ya kuendesha mitambo ya IPTL ambayo yameongezwa bei.

Nundu, anatuhumiwa kuingilia mchakato wa kumpata mzabuni wa kujenga gati namba 12 na 13 katika Bandari ya Dar es Salaam.

TAKUKURU YAOKOA SH. BILIONI 2

Tatika hatua nyingine, Takukuru imeokoa Sh. bilioni 2.45 kwa wakurugenzi wa majiji na manispaa mbalimbali nchini kwa kuwabana na kuwaamuru kuzirudisha baada ya kubainika kuwa zilitumika vibaya katika mwaka wa fedha 2009/2010.

Dk. Hoseah, alisema jitihada hizo zimefanywa na Takukuru baada ya kuwabana jumla wakurugenzi 87 kati yao 39 ndiwo wamerejesha fedha hizo Hazina.

Alisema wakurugenzi wengine 48 bado hawajarejesha fedha hizo na wataendelea kuwabana na wakishindwa kuzirudisha fedha hizo ifikapo mwishoni mwa mwezi huu watafikishwa mahakamani.

Dk. Hoseah alisema taasisi yake imekuwa ikifanya kazi kubwa katika kuokoa fedha za umma na kupambana na watu wanajihusisha na rushwa, lakini kuna baadhi ya watu wanaiona taasisi hiyo haifanyi kazi yoyote.

“Taasisi yangu inafanya kazi kubwa sana ndio maana tumeokoa kiasi hicho cha fedha na baadhi ya wakurugenzi  ambao hawajarejesha fedha hizo wanahaha wakitafuta pesa hizo kwa kuwa mwisho wa mwezi huu tutawapeleka mahakamani wakishindwa kulipa,” alisema Dk. Hoseah

TAHADHARI DHIDI YA MATAPELI

Wakati huo huo, Takukuru imewatahadharisha wananchi dhidi ya wimbi la matapeli ambao wamekuwa wakijifanya maafisa wa taasisi hiyo na kuwadanganya watu mbalimbali kuwa wanatuhuniwa kwa makosa ya rushwa na kuwadai hongo ili wawaachie.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na ofisi ya Uhusiano ya Takukuru jana, watu hao wamekuwa wakiwafuatilia baadhi ya watumishi wa umma waliotajwa katika ripoti ya CAG wakituhumiwa kwa makosa mbalimbali.

Taarifa hiyo ya Takukuru ilisema mtu yeyote atakayehitajika na Takukuru kwa uchunguzi au ushahidi watamuhita ofisini kwa utaratibu maalum kwa kuandikiwa barua au hati ya wito na siyo kuhojiwa mitaani kama matapeli hao wanavyofanya.

Taarifa hiyo imemtaka mtu mwenye kufahamu watu wa namna hiyo atoe taarifa katika ofisi za taasisi hiyo au polisi kwa kuwa matapeli hao wanaharibu sifa ya chombo hicho.

CHANZO: NIPASHE

Search This Blog