Kada
mmoja wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), amekufa papo hapo na wengine zaidi
ya 85 wamejeruhiwa vibaya baada ya lori aina ya Fuso lenye namba za
usajili T420 APM walilokuwa wakisafiria kwenda kwenye mkutano wa
uchaguzi wilayani Chunya kupinduka.
Ajali hiyo ilitokea jana majira ya saa
2:30 asubuhi katika eneo la Matundasi umbali wa kilometa 21 nje ya mji
wa Chunya, wakati wajumbe hao wa CCM zaidi ya 100 wakitokea katika kata
za Lupa, Upendo na Mamba kwenda kwenye mkutano wa uchaguzi.
NIPASHE ambalo lilifika kwenye eneo la
tukio na baadaye kwenye Hospitali ya Wilaya ya Chunya, lilishuhudia
magari ya kubeba wagonjwa zaidi ya matatu yakisomba majeruhi kuwatoa
eneo la ajali na kuwapeleka hospitalini, huku wengi wao wakiwa na
majeraha mabaya katika sehemu mbalimbali za miili yao.
Kaimu Mganga Mkuu wa Hospitali ya wilaya
ya Chunya, Dk. Henry Mwansasu, amethibitisha kutokea kwa ajali hiyo na
kudai kuwa amepokea mwili wa mtu mmoja pamoja na majeruhi 85.
Amemtaja mtu aliyepoteza maisha kwenye
ajali hiyo kuwa ni Issaya Nchimbi (45), ambaye ni Katibu wa Uchumi na
Fedha wa tawi la CCM la Madimbwini katika kata ya Mamba wilayani Chunya.
Alisema kati ya majeruhi hao, 11 hali zao
ni mbaya na wamelazwa hospitalini hapo kwa ajili ya matibabu na
uchunguzi zaidi, huku majeruhi wengine 63 ambao walipata mshtuko na
majeraha madogo madogo wakipatiwa matibabu na kuruhusiwa kurudi
nyumbani.
Akizungumza na gazeti hili katika
Hospitali ya wilaya ya Chunya, mmoja wa majeruhi hao, Bw. Frank Bone
(40), mkazi wa Lupa Tingatinga, alisema mbali na ajali hiyo kusababishwa
na dereva ambaye alitaka kupokea simu huku gari likiwa kwenye mwendo
mkali, pia gari hilo lilikuwa limajaza abiria kupita kiasi, hivyo muda
mwingi wa safari yao lilionekana kumshinda dereva.
Alisema kuwa waliianza safari yao kutoka
kijiji cha Mamba majira ya saa 9:00 usiku na kuwapitia wajumbe wengine
wa kata za Lupa na Upendo, ingawa gari lilijaa baadhi walining’inia
kwenye mabomba ya vyuma.
Mwingine aliyejeruhiwa paji la uso,
Jamson Mwaluka, mkazi wa kata ya Lupa, alisema kabla ya ajali dereva wa
gari hilo, aliyetajwa kwa jina moja la Mchungaji, alipigiwa simu na
ndicho chanzo cha ajali hiyo.
“Dereva alipigiwa simu iliyokuwa mfukoni,
wakati anahangaika kuitoa gafla alijikuta yuko kwenye kona na
alipojaribu kuliweka sawa ndipo gari lilipoteza muelekeo na kupinduka,”
alisema Mwaluka.
Kwa mujibu wa majeruhi hao, gari hiyo
ilibeba zaidi ya watu 100 ambao wote walikuwa ni wajumbe wa Mkutano Mkuu
wa uchaguzi wa CCM wilaya ya Chunya, kutoka kata tatu za Mamba, Lupa,
Tinga na Upendo katika jimbo la Lupa.
Hata hivyo, licha ya ajali kutokea,
mkutano wa uchaguzi uliendelea kama ulivyopangwa, huku baadhi ya
majeruhi walioruhusiwa kutoka hospitalini nao wakijumuika kushiriki
kwenye uchaguzi na wengine ambao wamelazwa wakiandaliwa utaratibu wa
kupiga kura wakiwa wodini.